MRENO Cristiano Ronaldo ameshinda tuzo ya Mwanasoka Bora wa Dunia wa mwaka wa FIFA kwa mara ya pili katika historia yake, akimuangusha mshindani wake mkuu, Lionel Messi.
Nyota huyo babu kubwa wa Real Madrid alikuwa anakabiliwa na ushindani wa mbali kidogo kwa nyota wa Barcelona, Messi na wa Bayern Munich, Franck Ribery katika kinyang’anyiro cha Ballon d’Or.
Akiwa mwenye hisia kali, Ronaldo aliyekwenda jukwaani kuchukua tuzo yake akiwa ameambatana na mtoto wake wa kiume, Cristiano alishindwa kujizuia na kumwaga machozi wakati anapokea taji hilo.

Namba 1: Cristiano Ronaldo ameshinda Ballon d’Or na kutajwa ndiye mwanasoka babu kubwa duniani

Mshindi: Pele akiwa amemshika mtoto wa Ronaldo, Cristiano wakati Mreno huyo anapokea tuzo yake
Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 28 amepewa tuzo hiyo baada ya kufunga mabao 66 katika mechi 56 za klabu na nchi yake, Ureno mwaka 2013 hatimaye kuirejesha tuzo yake aliyoitwaa awali mwaka 2008.
Pamoja na kwamba Ronaldo hakutwaa taji kubwa mwaka 2013, alifunga mabao yote manne Ureno ikiitoa Sweden katika kinyang’anyiro cha tiketi ya kombe la Dunia baadaye mwaka huu.
“Hakuna maneno ya kusema wakati huu,” Ronaldo alisema, huku akifuta machozi. ”Nataka kuwashukuru wenzangu wote na washirika pale Real Madrid, katika timu ya Ureno na familia yangu, ambako wako nami,”.
“Wale ambao wananifahamu mimi, wanafahamu kwamba watu wengi wananisaidia: kocha wangu, rais wetu, na sitaki kusahau kumtaja Eusebio. Mpenzi wangu na mwanangu pia. Nasonga zaidi,”.


No comments:
Post a Comment